WELCOME

MAY GOD BLESS YOU ALL FOR VISITING THIS SITE, A HOPE YOU WILL ENJOY EVERYTHING YOU GET HERE AND IF THERE Z ANYTHING BORING OR SHALLOW LEAVE COMMENTS PLEASE.
BE BLESSED

MY DIARY

My photo
Dar es Salaam, Tanzania, Tanzania
FRIEND TO EVERYONE AND I BELIEVE EVERYTHING IS POSSIBLE

RONNIE DOCOMENTARY

Popular Posts

Sunday, February 19, 2012

SITTA - MWAKYEMBE KALISHWA SUMU, POLISI WANAPOTOSHA

WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta ameendelea kusisitiza kwamba ugonjwa unaomsumbua Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, unatokana na kulishwa sumu. Kauli yake imekuja baada ya Jeshi la Polisi nchini kueleza kwamba ugonjwa unaomsumbua Naibu Waziri huyo hausababishwi na kula chakula chenye sumu; kauli iliyomuibua Dk. Mwakyembe na kudai Jeshi hilo halikumtendea haki akisema si lazima unyeshwe sumu ili ikudhuru. Sitta amesema, hoja ya Jeshi la Polisi kueleza kuwa suala hilo linahitaji ushahidi ni kuupotosha umma ili usielewe nini kinachomsumbua Dk. Mwakyembe ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kyela mkoani Mbeya. Akizungumza katika uzinduzi wa Asasi ya Kiraia ya Vijana wa Kanisa Katoliki mkoani Tabora (VITAL) uliofanyika kwenye Ukumbi wa Askofu Mkuu Marco Mihayo, Sitta ambaye ni Mbunge wa Urambo mkoani hapa, alisema yeye kama Waziri hawezi kusema uongo kuhusu jambo hilo. Alisema Jeshi la Polisi limekuwa likipotosha umma kukanusha kwamba Dk. Mwakyembe hajalishwa sumu ingawa Naibu Waziri huyo ana ushahidi wa kutosha kuhusu jambo hilo. “Mimi nitapigana hadi siku ya mwisho kutetea wanyonge na ninashangaa kuelezwa kwamba mimi nimeshitakiwa na Polisi kwamba nimepotosha umma kusema kwamba Dk. Mwakyembe amelishwa sumu. Na kwa taarifa yako Baba Askofu nimeelezwa jalada langu limepelekwa kwa Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP) ili nishitakiwe,” alisema Sitta. Alilishutumu Jeshi la Polisi kutokana na tabia ya kuhujumu watu na kusisitiza kuwa tabia hizo ni za kijambazi zinazoweza kuhatarisha hali ya usalama na maisha ya watu wanaozuliwa mashitaka kama hayo yanayomkabili. Akizungumza ufisadi, alisema amekuwa mstari wa mbele kupinga suala hilo kwa nguvu zote na atahakikisha anapigana kufa au kupona kupambana na watu wanaojilimbikizia mali kwa kutumia madaraka yao. Alisema jambo hilo halikubaliki na kwamba kwa sababu yupo hai, ataendelea kupambana nalo hadi hapo litakapoleta tija na hatimaye kuwawezesha wananchi wanufaike na rasilimali za nchi yao. Jeshi la Polisi kupitia Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Kamishna Robert Manumba, lilieleza kuwa kwa taarifa ilizopewa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na Hospitali ya Apollo nchini India, ni kwamba ugonjwa wa Dk. Mwakyembe haukutokana na kulishwa kitu chenye sumu. Lakini Dk. Mwakyembe katika taarifa yake juzi kwa vyombo vya habari hakueleza kwamba madaktari wamegundua kuwa amelishwa sumu, lakini akasema, “si lazima unyweshwe ili ikudhuru, inaweza kukudhuru hata kwa kugusishwa tu.” Alisema kwa mujibu wa taarifa ya madaktari wa Apollo, kuna kitu kwenye ujiuji wa ndani ya mifupa (bone marrow) kinachochea hali aliyonayo ambapo mabingwa wanahangaika kukifahamu. Sitta akizungumzia asasi aliyoizindua jana, alisema Serikali haina budi kuwaendeleza vijana na kuwawezesha ili wajishughulishe na shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwa ni mkakati wake wa kupambana na umasikini. Alieleza kwamba taifa lisiloangalia mustakabali wa vijana, linahatarisha usalama wake na kusababisha vitendo vya uhalifu vizidi kuongezeka kitu ambacho kinaweza kulifanya utawala wake uporomoke. Sitta alitoa kompyuta na printa yenye thamani ya Sh milioni moja na kuahidi kurejea tena kwa ajili ya kufanya harambee kubwa ambayo itasaidia kukusanya fedha kwa ajili ya asasi hiyo. Awali, Mwenyekiti wa Asasi hiyo, Deogratius Nzuki, alimueleza Waziri Sitta kwamba lengo la kuanzisha asasi hiyo ni kuwaunganisha vijana na kuwajenga kimaadili ili waitumikie nchi na Kanisa Katoliki vizuri.

Source: Habari Leo

No comments:

Post a Comment